Tuesday, September 11, 2012

HUKUMU YA KESI YA RUFAA YA GATETE KUTOLEWA OKTOBA 9


 
Na Hirondelle, Arusha
 
 
Arusha, Septemba 11, 2012 (FH) – Mahakama ya Rufaa ya Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (ICTR) Oktoba 9, 2012 itatoa hukumu ya kesi ya rufaa ya afisa mwandamizi wa zamani wa serikali ya Rwanda, Jean-Baptiste Gatete, kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Mahakama hiyo.
Katika kesi hiyo, pande zote mbili, za mwendesha mashitaka na utetezi zimekata rufaa dhidi ya hukumu iliyotolewa na mahakama ya awali Machi 29, 2011.
Gatete, ambaye ni Mkurugenzi wa zamani katika Wizara ya Wanawake na Masuala ya Familia alitiwa hatiani kwa mauaji ya kimbari na kutekekteza kizazi kama uhalifu dhidi ya binadamu na kuhukumiwa kifungo cha maisha jela.
Majaji walisikiliza rufaa hiyo Mei 7, mwaka huu huku upande wa mwendesha mashitaka ukiomba mtu huyo atiwe hatianin pia kwa kosa la kula njama. Kwa mujibu wa mwendesha mashitaka, mahakama ya awali imedaiwa kukosea kwa kutomtia hatiani Gatete kwa shitaka hilo kwa sababu karibu vigezo  vyote  vimefikiwa.
Lakini kwa upande wake, mawakili wa utetezi wameomba mteja wao aachiwe huru kwa mashitaka yote aliyotiwa nayo hatiani kwa madai kwamba hayakuthibitishwa. Upande wa utetezi pia umeomba kwamba iwapo  ombi lao la awali halitakubali basi mteja wao apunguziwe adhabu.
Katika mahakama ya awali, Gatete ilionekana na hatia pasipo mashaka yoyote kwa kuhusika na vifo vya mamia au hata maelfu ya Watutsi katika maeneo matatu yalikofanyikia mauaji hayo, Mashariki mwa Rwanda kati ya Aprili 7 na 12, 1994.
Maeneo yalikotokea umwagaji damu mkubwa ni pamoja na yale ya kata ya Rwankuba na parokia ya Kiziguro kwenye wilaya ya Murambi katika mkoa wa Byumba na maeneo ya parokia ya Mukarange katika wilaya ya Kayonza, mkoa wa Kibungo.
Gatete (59) alitiwa mbaroni nchini Congo-Brazzaville Septemba 11, 2002 na kisha kuhamishiwa makao makuu ya ICTR, Arusha nchini Tanzania. Kesi yake ilianza kusikilizwa Oktoba 20, 2009.

No comments:

Post a Comment