Friday, September 7, 2012

Halmashauri ya Meru yawapimia wananchi viwanja zaidi ya 4000 .




Halmashauri ya Meru yawapimia wananchi viwanja zaidi ya 4000 .
GLADNESS MUSHI, Arusha.
HALMASHURI ya Meru wilayani Arumeru mkoani Arusha imewapimia wananchi zaidi ya viwanja 4000  katika maeneo mbalimbali pamoja na kuwapatia michoro, ramani na hati za ardhi kwa lengo la kuwawezesha wananchi kuwa na usalama na mali zao.
Hayo yalisemwa hivi karibuni  na Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Meru, Godson Majola wakati akizungumza katika ufunguzi wa baraza la madiwani lililofanyika katika halmashauri hiyo.
Majola alisema kuwa , halmashauri hiyo wameandaa mikakati mbalimbali ya kuanza kuwapimia wananchi maeneo yao kwa lengo la kuwapatia hati miliki ili kuwawezesha kupata mikopo na hata kuendeleza shughuli mbalimbali za maendeleo katika maeneo yao.
Alisema kuwa, lengo la kuwapimia wananchi maeneo yao ni ili kuwawezesha kwa  urahisi kuaminika katika taasisi mbalimbali za fedha na kuweza kupata mikopo  , kwani changamoto kubwa iliyokuwa ikiwakabili ni kutokuwa na hati miliki za ardhi ambazo zinawawezesha kuchukua mikopo.
Alifafanua zaidi kuwa, upimaji huo wa ardhi za wananchi utafanyika kata zote za halmashauri hiyo ambapo mchakato huo tayari unaendelea  na  zoezi zima linaedelea vizuri katika maeneo mbalimbali.
Aidha aliwataka madiwani kuhakikisha wanashiriki  kikamilifu katika kutoa ushirikiano katika upimaji wa maeneo hayo ya wananchi ikiwa ni pamoja na kutatua changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika zoezi hilo.
Hata hivyo alitoa wito kwa viongozi mbalimbali ambao hawajawapimia wananchi maeneo yao kuhakikisha wanaanza mchakato huo mapema ili kuwawezesha wananchi hao kupata hati miliki ambazo zitawezesha kuchangia shughuli mbalimbali za maendeleo.
 ‘Jamani madiwani katika upimaji wa maeneo ya wananchi kunakuwepo na changamoto mbalimbali ndani yake lakini nyie ndio  mtakaowezesha kutatuliwa kwa changamoto hizo kwa wakati, hivyo wahusika wanapowafikia katika ameneo yenu tafadhali mtoe ushirikiano wa kutosha ili kila  mwananchi aweze kupata haki yake ya msingi’alisema Majola.
Naye Mkurugenzi wa halmashauri ya Meru,Trisias Kagenzi alisema kuwa, upimaji huo utawezesha kwa kiasi kikubwa sana kuondokana na ujenzi holela unaofanyika katika maeneo mengi ya  mji wa Usa river kwani kumekuwepo na wimbi kubwa sana la ujenzi holela katika maeneo mbalimbali.
Aidha alitumia fursa hiyo kuwataka madiwani wanasimamia kikamilifu miundombinu ya barabara hususani katika upanuzi wa barabara katika kata zao kwa lengo la kuhakikisha maendeleo yanakuwepo katika kata zao na kuweza kutatua changamoto mbalimbali za wanachi.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment