Wednesday, November 14, 2012

SHIRIKA LA POLISI LA KIMATAIFA KUSAIDIA EAC KUPAMBANA NA UHALIFU



Katika harakati za kuhakikisha kwamba Afrika Mashariki inaendelea kuwa salama kwa uwekezaji, Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC) na Shirika la Polisi la Kimataiafa(INTERPOL) wamekubaliana kushirikiana katika masuala ya usalama kwa manufaa ya pande zote mbili.

Katibu Mkuu wa EAC, Dk. Richard Sezibera alisema hayo alipokutana na kiongozi mwenzake wa INTERPOL, Roland Noble kwenye Mkutano wake Mkuu wa 18, mjini Roma, Italia, mwishoni mwa wiki, Shirika Huru la Habari la Afrika Mashariki linaripoti.

‘’Kadiri mtangamano wa EAC unavyozidi kujiimarisha na kupanuka, na uhuru unaopatikana kutokana na utekelezaji wa Itifaki ya Soko la Pamoja, mambo hasi ya uhalifu kama vile madawa ya kulevya, usafirishaji haramu wa binadamu, bidhaa feki na uhalifu wa mtandao nao unaongezeka na hivyo haunabudi kupigwa vita kwa nguvu zote,’’ alisisitiza Dk. Sezibera.
Katibu Mkuu huyo wa EAC aliongeza kwamba nafasi ya INTERPOL ina umuhimu wa pekee katika kusaidia EAC kutekeleza mikakati yake ya amani na usalama.
INTERPOL na EAC zinatarajiwa kutiliana saini mkataba wa maelewano kuhusu ushirikiano huo hivi karibuni.

Kwa mujibu wa taarifa ya Sekretariet ya EAC, majadiliano baaina ya taasisi hizo mbili juu ya masuala ya ushirikiano yalianza tangu mwaka 2009 kwa lengo la kutumia nafasi zilizopo kuimarisha ufanisi wa utendaji kazi katika taasisi hizo kwa masuala ya usalama katika kanda hiyo.
Kwa sasa nchi zote tano wanachama wa EAC; Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda na Burundi, zinawasiliana na INTERPOL katika ngazi ya ofisi ya kanda.

Wakati huo huo Rais wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo(IFAD) wenye makao yake makuu mjini Roma, Italia, Kanayo Nwanze amezihakikishia kuziunga mkono nchi wananchama wa EAC katika juhudi zke za kupambana na njaa ili kujitosheleza kwa chakula.

Alisema EAC itapewa kipaumbele cha kwanza katika mipango yake kwa mwaka 2013 na kuongeza kuwa maafisa waandamizi wa shirika lake wako tayari kujadili maeneo ya kushirikiana ili kuongeza uzalishaji wa chakula katika kanda hiyo.

Katika mazungumzo yao Dk. Sezibera alimweleza Rais huyo wa IFAD kwamba EAC imeandaa mpango mkakati wa kuiondoa hali tete inayojitokeza kila wakati ya kukosekana kwa usalama wa chakula.

No comments:

Post a Comment