Friday, November 9, 2012

ELIMU YA MAZINGIRA IANZIE KUANZIA NGAZI YA CHEKECHEA ILI KUOKOA JAMII DHIDI YA UHARIBIFU WA MAZINGIRA

ELIMU YA MAZINGIRA IANZIE KUANZIA NGAZI YA CHEKECHEA ILI KUOKOA JAMII DHIDI YA UHARIBIFU WA MAZINGIRA

Na MWANDISHI WETU, ARUSHA

IMEELEZWA kuwa endapo kama wanafunzi kuanzia ngazi ya madarasa ya awaali watafundishwa na kupewa mbinu za kutunza mazingira yanayowazunguka  basi wanafunzi hao watakuwa ni  wataalamu wazuri wa kutunza na kuthamini mazingira tofauti na sasa ambapo bado wapo baadhi ya wananchi wa maeneo mbalimbali ambao wanaharibu vibaya vyanzo vya mazingira kwa kushirikiana na watoto wao kwa kuwa hawana elimu ya kutosha huku watoto hao wakiona kuwa uharibifu wa mazingira ni jambo la  kawaida sana.

Wito huo umetolewa mjini Arusha na Mratibu wa shirika la Roots and Shoots,Bw Japhet Mwanangombe mapema wiki hii wakati akiongea na wanafunzi ambao ni wadau  wa mazingira (waelimishaji rika) zaidi ya 190 kutoka katika shule mbalimbali za msingi na Sekondari  kwa mkoa wa Arusha

Bw Mwanangombe alisema kuwa  kwa sasa  ni vema kama somo la elimu ya mazingira likafanywa kama somo lenye umuhimu mkubwa sana kwa wanafunzi kuanzia wale wa madarasa ya awali  kwa kuwa kama wanafunzi hao wataweza kupata vema elimu hiyo basi watakuwa ni mabalozi wazuri sana wa mazingira tofauti na sasa ambapo kwa  somo hilo linatolewa na wadau mbalimbali huku hata baadhi ya wazazi na wakuu wa shule wakiona kuwa ni moja ya elimu ambayo haina tija sana kwenye Jamii

Alisema kuwa elimu hiyo inapoanzia kuanzia ngazi ya chini kabisa itaweza kuwafanya watoto hata kuweza kuyapenda na kuyathamini mazingira ya Nchi na hivyo kukemea vikali sana suala zima la uharibifu wa mazingira ambapo mara nyingine unafanywa na wazazi au walezi wao kwa kuwa hawana elimu ya kutosha juu ya madhara ya uharibifu  huo.

“tuseme tusemavyo tuende tuendako  hii elimu ni ya muhimu sana kwenye Nchi yetu tena hususani Vijijini lakini kama tutakuwa tunaendelea kusema kuwa tuyapende mazingira huku hiki kizazi kikiwa hakiambiwi madhara ya uharibifu bado hatusaidii Jamii ila hawa watoto wetu wanatakiwa wapewe elimu hii ili kama hata wazazi wao  hawana elimu ya kutosha basi watawafundisha  wazazi wao  na hapo mazingira yataweza kuhifadhika tena hasa yale ya Vijijini,Aliongeza Bw Mwanangombe.

Mbali na hayo Mratibu huyo alisema kuwa nao wakuu wa shule wanatakiwa kuhakikisha kuwa wanatoa vipaumbele sanjari na uanzishwaji wa vitalu vya miti ndani ya shule zao na kuachana na tabia ya kuwakataza baadhi ya wanafunzi ambao wanamsukumo na suala zima la mazingira kwani kwa hali hiyo wanachangia sana uharibifu wa mazingira ambapo madhara kwa sasa yametanda sana ndani ya uso wa dunia.

Aliwataka wadau hao wa elimu ambao ni wakuu wa shule kuhakikisha kuwa kila shule inakuwa hata na mashindano ya kimazingira ambayo yataweza kuwapa wanafunzi fursa ya kuyapenda na kuthamini mazingira hasa kwa njia ya upandaji wa miti hali ambayo nayo itafanya jamii kuepukana na ukame ambao kwa sasa upo kwenye baadhi ya vijiji  na kutokana na ukame huo unasababisha hata vifo vya wanyama na mimea kukauka.

Nao wanafunzi hao walisema kuwa pamoja na kuwa Shirika hilo linawawezesha katika masuala mbalimbali hasa ya utunzaji wa mazingira basi jamii nayo hasa kupitia kwenye Familia zao na Serikali za mitaa zinatakiwa kuwapokea na kuacha tabia ya kuwadharau kutokana na kuwa na umri mdogo kwani kupitia kwao wanaweza kufanya mabadiliko makubwa sana katika sekta hiyo ya mazingira.

MWISHO.



No comments:

Post a Comment