Friday, December 14, 2012

WANANCHI WA ARUSHA VIJIJINI WAWATAKA MAAFISA MALI ASILI KUFIKA VIJIJINI NA KUACHA TABIA YA KUKAA MIJINI


WANANCHI WA ARUSHA VIJIJINI WAWATAKA MAAFISA MALI ASILI KUFIKA VIJIJINI NA KUACHA TABIA YA KUKAA MIJINI

Na Queen Lema, ARUSHA

IMEELEZWA kuwa kutokana na baadhi ya maafisa mali asili na mazingira kushindwa kufika vijijini kumesababisha vyanzo vingi vya mazingira kuendelea kuharibiwa ovyo na wananchi huku serikali ikiwa inadai mazingira yatunzwe

Asilimia kubwa ya watendaji hawa wa mazingira hawana mwitikio wa kuja vijijini na kuangalia vyanzo mbalimbali na badala yake wanafanya kazi zao wakiwa maofisini pekee hali ambayo inasababisha kila mara kuwepo na uharibifu wa mazingira

Kauli hiyo imetolewa na Wananchi wa wilaya ya Arusha Vijijini wakati wakiongea katika mdahalo unaohusiana na mabadiliko ya Tabia za Nchi uliofanyika chini ya mtandao wa asasi binafsi hapa mkoani Arusha (ANGONET)mapema jana.

Wananchi hao walisema kuwa kila siku ndani ya vyombo vya habari wanasikia kuwa wanatakiwa kutunza na kuthamini mazingira lakini bado elimu haiwafikii jamii hali ambayo bado ni sawa na kazi bure huku vijijini kukiwa na changamoto lukuki sana za uharibifu wa mazingira.

“suala la utunzaji wa mazingira bado ni suala tete sana ndani ya halmashauri hii ya Arusha vijijini kwa kuwa wananchi hatuna elimu hata kidogo ya mazingira na maafisa maliasili wetu wanakaa tu maofisini kwenye viyoyozi huku sisi tukiwa tunaambiwa kuwa tutunza mazingira na tuhakikishe kuwa tunakwepa uharibifu sasa sisi wa vijijini mara nyingine huwa tunaharibu mazingira kwa kuwa hatuna elimu lakini kama tungekuwa tunawaona hawa maafisa maliasili na mazingira basi vijijini tungekuwa na nafasi sana ya kuweza kutunza sana mazingira’waliongeza wananchi hao.

Awali Mratibu wa Mtandao wa asasi binafsi mkoani Arusha Bw Peter Bayo alisema kuwa lengo halisi la kufanya Mdahalo huo kwa Wilaya zote za mkoa wa Arusha ni kuhakikisha kuwa wananchi hasa wa vijijini wanakuwa na uelewa halisi wa masuala ya mazingira kwani bado mabadiliko ya Tabia za nchi yanaathiri sana maendeleo ya Jamii.

Bw Bayo alisema kuwa bado kuna changamoto kubwa sana ya uharibifu wa mazingira hususani ya maeneo ya  vijijini ambapo baadhi ya Sera za mazingira na misitu hazifuatwiu na watendaji wa Serikali hali ambayo inachangia sana kukitihiuri kwa mabadiliko ya tabia za nchi.

‘suala la mazingira linaendana na uchumi sasa bado kuna uhitaji mkubwa sana wa kuhakikisha wananchi hasa wale wa vijijini wanakuwa na elimu ingawaje changamoto kubwa sana kwa sasa ni baadhi ya watendaji kushindwa kufika vijijini kutokana na uhaba wa usafiri”aliongeza Bw Bayo

Naye afisa misitu katika halmashauri ya Arusha Vijijini Bw Semu Sikawa alisema kuwa wanauhitaji mkubwa sana wa kufika Vijijini kusaidia jamii dhidi ya mabadiliko ya tabia za nchi lakini kitu kikubwa kinachowakamisha ni uhaba wa vifaa vya kazi,pamoja na uhaba wa watumishi hali ambayo inawafanya washindwe kufika vijijini

MWISHO

No comments:

Post a Comment