Friday, December 14, 2012

BARAZA LA MICHEZO TANZANIA LAWATAKA WADAU WA MICHEZO KUJITOKEZA


Joseph Ngilisho,Arusha
 
BARAZA la michezo Tanzania BMT,limewataka wadau wa michezo kote nchini kujitokeza kwa wingi kushiriki program inayolenga kukusanya maoni juu ya rasimu ya namna ya kuhamasisha na kuendeleza michezo shirikishi  hapa nchini .
 
Akizungumza kwenye warsha ya kukusanya maoni jijini 
Arusha,Afisa mwandamizi wa BMT ,John Chalukulu alisema kuwa lengo la kukusanya maoni kwa wadau wa michezo hapa nchini ni kuhakikisha kuwa michezo inapendwa na jamii kwani kwa kiwango kikubwa jamii imeipa kisogo.
 
Alisema kuwa kwa sasa kumekuwepo na mwamko hafifu kwa jamii kuhusu suala la michezo na kwa kubaini hilo wameamua kuanzisha midahalo katika mikoa mitano hapa nchini itakayowakutanisha wadau wa michezo ili kubaini jamii inahitaji nini kukuza michezo hapa nchini.
 
Akizungumzia hali ya kudorora kwa sekta ya michezo hapa nchi alisema kumekuwapo na changamoto nyingi ikiwemo ukosefu wa fedha,mwamko hafifu wa kushiriki michezo,wananchi kupenda michezo ya aina moja nk,ukosefu wa viwanja vya michezo pamoja na vifaa.
 
Kwa upande wa mgeni rasmi katika warsha hiyo,Sifael Ole Ngashwa Mollel ambaye ni kaimu katibu tawala wa wilaya,alilitaka baraza hilo la michezo nchini kujikita kuhamasisha zaidi michezo mashuleni ili jamii ione umuhimu wa kutoa kipaumbele kwenye sekta hiyo.
 
Alisema kuwa, swala la michezo linapaswa kufanyika kwa umakini zaidi huku wakiwafikia walengwa ambao ni wanafunzi wa shule za msingi ,vyuo vikuu na taasisi zote ili kuwezesha kupata wataalamu katika ngazi zote na hatimaye kuwezesha elimu ya michezo kuenea ngazi zote.
 
 ‘’pelekeni walimu wa michezo mashuleni na muongeze hamasa ili jamii ianze kuona umuhimu wa kutoa kipaumbele masuala ya michezo kwa vijana na makundi mengine kwani hivi sasa michezo imezorota sana mashuleni kutokana na kutokuwa na walimu wenye uzoefu wa kutosha ambao wana uwezo wa kutoa elimu hiyo’’alisema.
 
Aliongeza kuwa, swala la michezo katika shule mbalimbali hivi sasa limekuwa likifanyika kwa kuigiza hali  ambayo imechangia kupotea kwa maana halisi ya michezo mashuleni ,hivyo baraza hilo lina changamoto kubwa kuhakikisha kuwa linajiwekea mikakati na utaratibu mzuri wa kuandaa michezo mashuleni .
 
Mollel aliongeza kuwa, umefika wakati sasa wa halmashauri zote nchini kuhakikisha kuwa zinashirikiana na baraza hilo kutatua changamoto mbalimbali ikiwemo upatikanaji wa viwanja, katika shule mbalimbali za msingi ili kuwezesha wanafunzi kupata haki zao za msingi.
 
BMT,tayari imeshaifikia mikoa ya Zanzibar,Mwanza na Arusha ikifuatiwa na mikoa ya Songea na Dar es salaam.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment