Saturday, March 9, 2013

UKOSEFU WA NYUMBA ZA POLISI MERERANI CHANZO CHA UTENDAJI HAFIFU WA POLISI


UKOSEFU WA NYUMBA ZA POLISI MERERANI CHANZO CHA UTENDAJI HAFIFU WA POLISI


IMEELEZWA kuwa ukosefu wa nyumba za askari polisi wa kituo cha Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara unachangia kuchelewesha utendaji kazi wao kwani inawabidi watoke majumbani kwao na kwenda kituoni ndipo wafike kwenye eneo la tukio.

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Mamlaka ya Mji mdogo wa Mirerani,Albert Siloli kwenye kikao cha siku ya familia ya polisi na wadau wa mji huo cha kujadili tathmini ya utendaji kazi wake kwa mwaka uliopita.

Siloli alisema ukosefu wa nyumba za askari polisi unachangia kwa kiasi kikubwa kudhoofisha utendaji kazi wao kwani unawachelewesha kufika kwenye tukio husika na kuchukua hatua stahili ikiwemo kuthibiti uhalifu.

Alisema Serikali inapaswa kulipatia ufumbuzi tatizo hilo kwa kuwajengea nyumba karibu na kituo cha polisi askari hao ili waweze kutimiza wajibu wao kwa jamii ipasavyo kwani hivi sasa mji huo unazidi kupanuka kwa haraka.

Hata hivyo,kwa niaba ya wenyeviti wengine wa mitaa ya mji mdogo wa Mirerani,Siloli alitoa pongezi kwa askari hao kwani uhalifu hivi sasa umepungua kwa kiasi kikubwa kwenye mji wa Mireraani hivyo jamii inaishi kwa amani ya kutosha.   

Pia,Mwenyekiti huyo alimpongeza Mkuu wa kituo cha polisi Mirerani,Mrakibu Msaidizi wa polisi Ally Mohamed Mkalipa kwa kuandaa hafla kwani haijawahi kufanyika tangu kituo hicho kianzishwe mwaka 1998 na utendaji kazi wao ni wa asilimia 100.

Pamoja na hayo alisema baadhi ya askari wa usalama barabarani wanakabiliwa na changamoto ya kudaiwa kupokea rushwa kwenye kazi zao hivyo kulitia doa jeshi hilo kwani jamii inalalamika mno kuhusiana na jambo hilo.

Kwa upande wake,Mkuu wa kituo cha Polisi Mirerani Mrakibu Msaidizi wa polisi (ASP) Ally Mohamed Mkalipa aliwashukuru wenyeviti wa mitaa hao kwa kutambua kuwa uhalifu hivi sasa umepungua kwenye mji huo.

Mkalipa ameeleza kuwa jamii inatakiwa kuongeza ushirikiano kwao kwani ni dhahiri shahiri uhalifu umepungua kwa kiasi kikubwa na watajitahidi kuondokana na changamoto zinazowakabili

Kuhusu suala la baadhi ya askari polisi kuhusishwa na upokeaji rushwa amesema watalifuatilia jambo hilo kwani maadili yanawataka askari  wasijihusishe na vitendo.

Alisema kisingizio cha kudai kuwa mshahara mdogo unachangia polisi kupokea rushwa siyo sahihi kwani upo utafiti umebaini kuwa hata wanaopokea mshahara mkubwa wana kawaida ya kupokea rushwa hivyo watawachunguza na wakiwabaini watawachukulia hatua ikiwemo kuwashitaki kijeshi,kuwafukuza kazi na kwenye mahakama za kawaida.

MWISHO.

No comments:

Post a Comment